Kweli kifo ni mwisho wa mambo yote?
Watu wengi hawapendi kuzungumza kuhusu kifo. Lakini wakati fulani, lazima sisi sote tukabiliane nacho. Kifo husababisha uchungu mwingi sana.
Hatuwezi kujitayarisha vya kutosha kwa ajili ya
kifo cha mzazi, mwenzi wa ndoa, au mtoto. Kifo kinaweza kutokea ghafula
au kutokea polepole. Vyovyote vile, uchungu wa kifo hauwezi kuepukwa, na
unaweza kuumiza sana.
Antonio, ambaye baba yake alikufa katika
aksidenti, anaeleza: “Kifo ni kama mtu anayefunga mlango wako na kwenda
na funguo. Huwezi kuufungua hata kidogo. Unabaki tu na kumbukumbu. Huo
ndio ukweli wa mambo. Huenda ukakataa ukweli huo, kwa sababu unahisi
kwamba ni ukosefu wa haki, lakini huwezi kufanya lolote.”
Dorothy aliyefiwa na mumewe akiwa na umri wa miaka
47, aliazimia kutafuta majibu ya maswali fulani. Alipokuwa mwalimu wa
kuwafundisha watoto Biblia siku ya Jumapili, hakuamini kifo ni mwisho wa
mambo yote. Lakini kwa kweli, hakujua kinachotukia baada ya mtu kufa.
Alimwuliza kasisi Mwanglikana hivi: “Ni nini hutupata baada ya kufa?”
Kasisi huyo alimjibu: “Hakuna anayejua. Tukifa tutajua.”
Je, tusubiri mpaka tufe ili tujue kinachotukia? Je, kuna njia nyingine ya kujua ikiwa kwa kweli kifo ni mwisho wa mambo yote?
Kipengele: Mafundisho
0 Maoni