Alijifunza Kutii
BABA anasimama dirishani na
kumtazama mwana wake akicheza na
rafiki zake. Mpira wao unadunda na
kwenda barabarani. Mvulana huyo
anautazama na hajui atafanya nini.
Rafiki yake mmoja anamhimiza
aufuate mbio barabarani. Hata hivyo,
mvulana huyo anatikisa kichwa chake
na kusema: “Siruhusiwi kufanya
hivyo.” Baba yake anafurahi.
2 Kwa nini baba huyo amefurahi?
Kwa sababu amemfundisha mwana
wake asiende barabarani akiwa peke
yake. Mvulana huyo anapotii, ingawa
hajui kwamba baba yake
anamtazama, baba yake anajua
kwamba mwana wake anajifunza
kutii na hivyo atakuwa salama. Baba
huyo anahisi kama Baba yetu wa
mbinguni, Yehova. Mungu anajua
kwamba ili tuendelee kuwa
waaminifu na kuona wakati ujao
mzuri ambao ametuahidi, lazima
tujifunze kumtegemea na kumtii.
(Methali 3:5, 6 ) Ndiyo sababu
alitutumia mwalimu bora zaidi kati
ya walimu wote wa kibinadamu.
3 Biblia inasema jambo fulani
lenye kushangaza kumhusu Yesu:
“Ijapokuwa yeye alikuwa Mwana,
alijifunza kutii kutokana na mambo
aliyoteseka; na baada ya yeye
kufanywa kuwa mkamilifu akawa
ndiye mwenye daraka la wokovu wa
milele kwa wale wote
wanaomtii.” (Waebrania 5:8, 9 )
Mwana huyo alikuwa ameishi kwa
miaka mingi mbinguni. Alimwona
Shetani na malaika wenzake wakaidi
wakiasi, lakini Mwana huyo mzaliwa
wa kwanza hakuwaunga mkono.
Unabii ulioongozwa na roho ulisema
hivi kumhusu: “Sikuwa
mwasi.” ( Isaya 50:5 ) Basi, maneno
haya “alijifunza kutii” yanamhusu
namna gani Mwana huyo aliyetii
kikamilifu? Kiumbe huyo mkamilifu
‘angefanywa kuwa mkamilifu’ jinsi
gani?
4 Fikiria mfano huu. Askari ana
upanga wa chuma. Ingawa
haujatumiwa vitani, umetengenezwa
vizuri kabisa. Hata hivyo,
anabadilisha upanga huo na kutumia
mwingine uliotengenezwa kwa chuma
kigumu zaidi. Upanga huo wa pili
tayari umetumiwa sana vitani. Je, si
jambo la hekima kutumia upanga
huo wa pili badala ya ule wa
kwanza? Vivyo hivyo, Yesu alitii
kikamilifu kabla ya kuja duniani.
Lakini baada ya kukaa hapa duniani,
utii wake ukawa tofauti kabisa.
Ulijaribiwa, ulitiwa nguvu, na
kuthibitishwa kwa majaribu ambayo
Yesu hangekabili akiwa mbinguni.
5 Utii ni sifa ya maana ambayo
Yesu alihitaji alipokuja duniani.
Akiwa “Adamu wa mwisho,” Yesu
alikuja kufanya kile ambacho mzazi
wetu wa kwanza hakufanya, yaani,
kuendelea kuwa mtiifu kwa Yehova
Mungu, hata chini ya jaribu.
(1 Wakorintho 15:45 ) Hata hivyo,
Yesu hakutii kidesturi tu. Yesu alitii
kwa akili yake yote, moyo wake wote,
na nafsi yake yote. Naye alifanya
hivyo kwa shangwe. Kufanya mapenzi
ya Baba yake kulikuwa jambo la
maana kwake kuliko kula! ( Yohana
4:34 ) Ni nini kitakachotusaidia tuwe
watiifu kama Yesu? Acheni kwanza
tuchunguze mambo yaliyomchochea
kutii. Kuchochewa na mambo hayo
kutatusaidia kupinga vishawishi na
kufanya mapenzi ya Mungu. Kisha,
tutazungumzia thawabu fulani za
kuonyesha utii kama wa Kristo.
Mambo Yaliyomchochea Yesu
Kutii
6 Utii wa Yesu ulitokana na
mambo yaliyokuwa moyoni mwake.
Kama tulivyoona katika Sura ya 3,
Kristo alikuwa mnyenyekevu moyoni.
Kiburi kinafanya watu wachukie kutii,
lakini unyenyekevu unatusaidia
kumtii Yehova kwa hiari. (Kutoka 5:1,
2; 1 Petro 5:5, 6 ) Isitoshe, utii wa
Yesu ulitokana na yale aliyopenda na
yale aliyochukia.
7 Zaidi ya yote, Yesu alimpenda
Baba yake wa mbinguni, Yehova.
Katika Sura ya 13, upendo huo
utazungumziwa kwa mapana na
marefu. Upendo huo ulimfanya Yesu
amwogope Mungu. Alimpenda na
kumheshimu sana Yehova, Baba
yake, hivi kwamba aliogopa
kumchukiza. Kumwogopa Mungu ni
sababu moja iliyofanya sala za Yesu
zisikiwe vizuri. ( Waebrania 5:7 ) Pia,
kumwogopa Yehova ni jambo moja
linaloonekana wazi katika utawala wa
Yesu akiwa Mfalme wa Kimasihi.—
Isaya 11:3 .
8 Kumpenda Yehova kunatia
ndani kuchukia mambo ambayo
Yehova anachukia. Kwa mfano, ona
unabii huu unaoelekezwa kwa
Mfalme wa Kimasihi: “Umependa
uadilifu nawe unachukia uovu. Ndiyo
sababu Mungu, Mungu wako,
amekutia mafuta kwa mafuta ya
kushangilia kuliko wenzako.” (Zaburi
45:7 ) ‘Wenzake’ Yesu ni wale
wafalme wengine katika ukoo wa
Mfalme Daudi. Yesu anapotiwa
mafuta, anakuwa na sababu ya
kushangilia sana kuliko yeyote kati
yao. Kwa nini? Thawabu yake ni
kubwa kuliko yao, na faida za ufalme
wake ni nyingi kupita zile za falme
zao. Anapewa thawabu kwa sababu
kupenda uadilifu na kuchukia uovu
kulimchochea amtii Mungu katika
mambo yote.
9 Ni kwa njia gani Yesu
alionyesha maoni yake kuhusu
uadilifu na uovu? Kwa mfano, Yesu
alihisi namna gani wakati wafuasi
wake walipotii maagizo yake katika
kazi ya kuhubiri na hivyo kupata
baraka? Alijawa na shangwe. ( Luka
10:1, 17, 21 ) Na watu wa Yerusalemu
walipokosa kutii tena na tena, na
kukataa jitihada zake zenye upendo
za kuwasaidia, Yesu alihisi namna
gani? Alilia kwa sababu ya uasi wa
jiji hilo. (Luka 19:41, 42) Yesu
alipendezwa sana na mwenendo
mzuri na kuchukizwa na mwenendo
mbaya.
10 Kutafakari kuhusu maoni ya
Yesu kunatusaidia kuchunguza yale
yanayotuchochea sisi binafsi kumtii
Yehova. Ingawa sisi si wakamilifu,
tunaweza kujizoeza kupenda mema
kutoka moyoni na kuchukia kabisa
mwenendo mbaya. Tunahitaji kusali
kwa Yehova, na kumwomba atusaidie
kusitawisha maoni kama yake na ya
Mwana wake. (Zaburi 51:10 ) Wakati
huohuo, tunapaswa kuepuka mambo
yanayoweza kuchafua akili zetu.
Tunapaswa kuchagua burudani na
marafiki kwa uangalifu. (Methali
13:20; Wafilipi 4:8 ) Tukichochewa na
mambo yaliyomchochea Kristo,
hatutatii kidesturi tu. Tutatenda
mema kwa sababu tunapenda
kufanya hivyo. Tutaepuka kutenda
mabaya, si kwa sababu tunaogopa
kugunduliwa, bali kwa sababu
tunachukia mwenendo huo.
“Hakufanya Dhambi”
11 Mapema katika huduma yake,
Yesu alijaribiwa kuhusiana na
kuchukia dhambi. Baada ya
kubatizwa, alikaa nyikani siku 40
mchana na usiku, bila chakula.
Mwishoni mwa kipindi hicho, Shetani
alikuja kumshawishi. Ona jinsi Ibilisi
alivyotumia ujanja.— Mathayo 4:1-11 .
12 Shetani alianza kwa kusema:
“Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu,
yaambie mawe haya yawe
mikate.” (Mathayo 4:3 ) Yesu alihisi
namna gani baada ya kufunga kwa
muda mrefu? Biblia inasema wazi:
‘Aliona njaa.’ ( Mathayo 4:2 ) Kwa
hiyo, Shetani alitumia tamaa ya
kiasili ya kutaka kula, na inaonekana
alingoja kimakusudi mpaka Yesu
alipokuwa dhaifu kimwili. Fikiria pia
maneno haya ambayo Shetani
alitumia kumdhihaki: “Ikiwa wewe ni
mwana wa Mungu.” Shetani alijua
kwamba Yesu ni “mzaliwa wa kwanza
wa viumbe vyote.” ( Wakolosai 1:15 )
Hata hivyo, Yesu hakumruhusu
Shetani amchochee kuasi. Yesu
alijua kwamba si mapenzi ya Mungu
atumie nguvu zake kwa makusudi ya
ubinafsi. Alikataa kufanya hivyo,
akionyesha kwamba anamtegemea
Yehova kwa unyenyekevu ili
amtegemeze na kumwongoza.—
Mathayo 4:4 .
13 Katika kishawishi cha pili,
Shetani alimpeleka Yesu juu ya
mnara wa hekalu. Akilipindua Neno
la Mungu kwa werevu, Shetani
alimshawishi Yesu afanye tamasha ya
kujionyesha kwa kujirusha chini
kutoka kwenye mnara huo ili malaika
wamwokoe. Ikiwa umati uliokuwa
hekaluni ungeona muujiza huo, je,
baada ya kisa hicho kuna mtu yeyote
ambaye angejaribu kutilia shaka
kwamba Yesu ni Masihi
aliyeahidiwa?
Na ikiwa umati
ungemkubali Yesu kuwa Masihi kwa
sababu ya muujiza huo, je, Yesu
hangekuwa ameepuka matatizo
mengi? Pengine. Lakini Yesu alijua
kwamba Yehova alimtaka Masihi
afanye kazi yake kwa unyenyekevu,
bali si kuwashawishi watu
wamwamini kwa kufanya tamasha
kubwakubwa. (Isaya 42:1, 2 ) Kwa
mara nyingine tena, Yesu alikataa
kumwasi Yehova. Hakunaswa na
mtego wa umashuhuri.
14 Namna gani mtego wa
mamlaka? Katika kishawishi chake
cha tatu, Shetani aliahidi kumpa
Yesu falme zote za ulimwengu ikiwa
tu Yesu angefanya tendo moja la
kumwabudu Shetani. Je, Yesu
alifikiria kwa uzito ahadi hiyo ya
Shetani? Alimjibu: “Nenda zako,
Shetani!” Kisha akaongeza: “Kwa
maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu
wako ndiye unayepaswa kumwabudu,
na yeye peke yake ndiye unayepaswa
kumtolea utumishi
mtakatifu.’” (Mathayo 4:10 ) Hakuna
chochote ambacho kingeweza
kumshawishi Yesu aabudu mungu
mwingine. Hakuna ahadi yoyote ya
kupata mamlaka au uwezo katika
ulimwengu huu ambayo ingeweza
kumshawishi afanye tendo lolote la
uasi.
15 Je, Shetani alikubali
kushindwa? Aliondoka alipofukuzwa
na Yesu. Hata hivyo, Injili ya Luka
inasema kwamba Ibilisi ‘alimwacha
mpaka wakati mwingine
unaofaa.’ ( Luka 4:13 ) Bila shaka,
Shetani angepata nafasi nyingine za
kumjaribu na kumshawishi Yesu,
mpaka mwisho. Biblia inatuambia
kwamba Yesu ‘alijaribiwa katika
mambo yote.’ (Waebrania 4:15 ) Kwa
hiyo, Yesu alipaswa kuwa macho
sikuzote; nasi tunapaswa kufanya
vivyo hivyo.
16 Hata leo hii, Shetani
anawashawishi watumishi wa
Mungu. Inasikitisha kwamba
kutokamilika kwetu kunafanya iwe
rahisi kushambuliwa. Shetani
anatumia kwa ujanja mwelekeo wetu
wa kuwa na ubinafsi, kiburi, na
tamaa ya mamlaka. Akitumia mtego
wa kufuatia vitu vya kimwili, Shetani
anaweza hata kutumia mambo yote
hayo kwa safari moja! Tunapaswa
tujichunguze kwa unyoofu mara kwa
mara. Tunapaswa kutafakari maneno
ya 1 Yohana 2:15-17 . Tunapofanya
hivyo, tunaweza kujiuliza iwapo
tamaa za kimwili za mfumo huu wa
mambo, tamaa ya mali, na tamaa ya
kuwapendeza wengine imedhoofisha
kwa kiasi fulani upendo wetu kwa
Baba yetu wa mbinguni. Tunahitaji
kukumbuka kwamba ulimwengu huu
utaangamizwa, na ndivyo na mtawala
wake, Shetani. Na tukatae katakata
hila zake za kutushawishi
tutumbukie katika dhambi! Acheni
tuchochewe na Bwana wetu, kwa
maana “hakufanya dhambi.”— 1 Petro
2:22 .
“Sikuzote Mimi Hufanya
Mambo Yanayompendeza”
17 Kutii kunatia ndani mengi
zaidi kuliko kuepuka dhambi; Kristo
alitimiza amri zote za Baba yake.
Alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya
mambo yanayompendeza.” (Yohana
8:29 ) Utii huo ulimletea Yesu
shangwe nyingi. Bila shaka, wengine
wanaweza kudai kwamba haikuwa
vigumu kwa Yesu kutii. Labda
wanafikiri kwamba alipaswa kumtii
Yehova tu, ambaye ni mkamilifu, hali
sisi tunalazimika kuwatii wanadamu
wasio wakamilifu walio na mamlaka.
Hata hivyo, ukweli ni kwamba, Yesu
alikuwa mtiifu kwa wanadamu wasio
wakamilifu waliokuwa na mamlaka.
18 Alipokuwa akikua, Yesu alikuwa
chini ya mamlaka ya Yosefu na
Maria, wazazi wake wa kibinadamu
ambao hawakuwa wakamilifu.
Inaonekana kwamba angeweza kuona
makosa ya wazazi wake hata kuliko
watoto wengine. Je, aliasi, akivuka
mipaka iliyowekwa na Mungu kwa
ajili ya watoto na kuanza kuwaambia
jinsi ya kusimamia familia? Ona jinsi
andiko la Luka 2:51 linavyosema
kumhusu Yesu, alipokuwa na umri
wa miaka 12: “Akaendelea kujitiisha
kwao.” Kwa kutii, aliwawekea mfano
mzuri vijana Wakristo, ambao
wanawatii wazazi wao na kuwapa
heshima wanayostahili.— Waefeso
6:1, 2 .
19 Kwa habari ya kutii wanadamu
wasio wakamilifu, Yesu alikabili hali
fulani ngumu ambazo Wakristo wa
kweli leo hawakabili. Fikiria hali
zisizo za kawaida ambazo zilikuwapo
nyakati alizoishi. Kwa muda mrefu,
Yehova alikuwa ameukubali mfumo
wa mambo wa dini ya Kiyahudi
pamoja na hekalu lake huko
Yerusalemu na ukuhani wake. Hata
hivyo, baada ya muda usio mrefu,
mfumo huo ungeondolewa mbali na
mahali pake pachukuliwe na mpango
wa kutaniko la Kikristo. (Mathayo
23:33-38 ) Kabla ya hatua hiyo
kuchukuliwa, viongozi wengi wa dini
walikuwa wakifundisha uwongo
uliotokana na falsafa ya Kigiriki.
Ufisadi ulikuwa umeenea sana
hekaluni hivi kwamba Yesu aliliita
“pango la wanyang’anyi.” ( Marko
11:17 ) Je, Yesu alikataa kwenda
katika hekalu hilo na masinagogi?
Hapana! Bado Yehova alikuwa
akitumia mipango hiyo. Mpaka
wakati Mungu alipochukua hatua na
kufanya mabadiliko, Yesu aliendelea
kutii kwa kwenda katika sinagogi na
kuhudhuria sherehe hekaluni.— Luka
4:16; Yohana 5:1 .
20 Ikiwa Yesu alikuwa mtiifu
katika hali hizo, basi Wakristo wa
kweli wanapaswa kuwa watiifu hata
zaidi leo! Tunaishi katika hali tofauti
kabisa, katika enzi zilizotabiriwa
zamani sana ambapo ibada safi
ingerudishwa.
Mungu
anatuhakikishia kwamba
hatamruhusu Shetani awapotoshe
watu wake waliorudishwa. (Isaya 2:1,
2; 54:17 ) Ni kweli kwamba katika
kutaniko la Kikristo tunakabiliana na
dhambi na watu ambao si
wakamilifu. Lakini, je, tunapaswa
kuyatumia makosa ya wengine kuwa
kisingizio cha kutomtii Yehova, labda
kwa kutohudhuria mikutano ya
Kikristo au kuwachambua wazee?
Hatupaswi! Badala yake, tunawaunga
mkono kwa moyo wote wale
wanaoongoza kutanikoni. Tunatii kwa
kuhudhuria mikutano na
makusanyiko ya Kikristo na kutumia
mashauri ya Kimaandiko tunayopata
katika pindi hizo.— Waebrania 10:24,
25; 13:17 .
21 Yesu hakuwaruhusu watu, hata
rafiki zake waliomtakia mema,
wamzuie asimtii Yehova. Kwa mfano,
mtume Petro alijaribu kumsadikisha
Bwana wake kwamba haikuwa lazima
ateseke na kufa. Ingawa Petro
hakuwa na nia mbaya alipomshauri
Yesu ajitendee kwa fadhili, Yesu
alikataa kabisa shauri hilo lisilofaa.
(Mathayo 16:21-23 ) Leo, wafuasi wa
Yesu hukabiliana na watu wa ukoo
ambao, ingawa hawana nia mbaya,
wanaweza kujaribu kuwashawishi
wasitii sheria na kanuni za Mungu.
Kama vile wafuasi wa Yesu wa karne
ya kwanza, msimamo wetu ni
kwamba “lazima tumtii Mungu kuwa
mtawala kuliko wanadamu.”—
Matendo 5:29 .
Thawabu za Kuwa Watiifu
Kama Kristo
22 Yesu alipokaribia kufa, utii
wake ulijaribiwa vikali zaidi. Siku
hiyo ya mwisho na ya majonzi
‘alijifunza utii’ kikamili. Alifanya
mapenzi ya Baba yake, si yake
mwenyewe. ( Luka 22:42 ) Kwa kufanya
hivyo, aliweka mfano mzuri wa
utimilifu. ( 1 Timotheo 3:16 ) Alijibu
swali lililotokezwa zamani za kale: Je,
mwanadamu mkamilifu anaweza
kuendelea kumtii Yehova
anapojaribiwa? Adamu alishindwa,
na Hawa vilevile. Kisha Yesu akaja,
akaishi, akafa, na hivyo kujibu swali
hilo. Yule aliye mkuu zaidi kati ya
viumbe wote wa Yehova alitoa jibu la
kukata maneno. Alitii hata wakati
ambapo utii ulifanya ateseke sana
na hata kufa.
23 Utimilifu, au kujitoa kwa
Yehova kwa moyo wote, unaonyeshwa
kupitia utii. Kwa kuwa Yesu alitii,
aliendelea kuwa mtimilifu na
kuwafaidi wanadamu wote. ( Waroma
5:19 ) Yehova alimpa Yesu thawabu
kubwa sana. Tukimtii Bwana wetu,
Kristo, Yehova atatupa thawabu pia.
Kumtii Kristo kunatuwezesha kupata
“wokovu wa milele.”— Waebrania 5:9 .
24 Isitoshe, utimilifu wenyewe ni
thawabu. Andiko la Methali 10:9
linasema: “Anayetembea kwa
utimilifu atatembea salama.” Ikiwa
utimilifu ungelinganishwa na
nyumba kubwa ya matofali yenye
kupendeza, kila tendo la utii
linaweza kulinganishwa na tofali
mojamoja. Mtu anaweza kufikiri
kwamba tofali moja halina maana,
lakini kila moja lina mahali pake na
kazi yake. Na matofali mengi
yanapounganishwa pamoja, jengo
lenye thamani hata zaidi
linatokezwa. Matendo ya utii
yanapowekwa pamoja, siku baada ya
siku na mwaka baada ya mwaka,
tunajenga nyumba yenye kupendeza
ya utimilifu wetu.
25 Utii wa muda mrefu
unatukumbusha sifa nyingine, yaani,
uvumilivu. Sifa hiyo ya Yesu
itazungumziwa katika sura
inayofuata.
Unaweza Kumfuata Yesu Jinsi Gani?
● Baadhi ya amri za Kristo ni zipi,
tunaweza kuzitii jinsi gani, nasi
tutapata baraka gani kwa kuzitii?—
Yohana 15:8-19 .
● Mwanzoni, watu wa ukoo wa Yesu
walikuwa na maoni gani kuhusu
huduma yake, nasi tunaweza
kujifunza nini kutokana na jinsi
alivyoshughulika nao?— Marko
3:21, 31-35 .
● Kwa nini hatupaswi kuogopa
kwamba tukimtii Yehova tutakosa
furaha maishani?—Luka 11:27, 28 .
● Tunaweza kujifunza nini kutokana
na utayari wa Yesu wa kutii sheria
ambayo haikuwa lazima aitii?—
Mathayo 17:24-27
Kipengele: Habari mpya, Ujumbe wa leo


0 Maoni