Je, Biblia Ina Ujumbe wa Siri?
MIAKA miwili hivi baada ya Waziri
Mkuu wa Israeli Yitzhak Rabin kuuawa mwaka wa 1995, mwandishi mmoja wa
habari alidai kwamba kwa kutumia kompyuta amegundua utabiri wa mauaji
hayo ukiwa umefichika katika maandishi ya awali ya Kiebrania ya Biblia.
Mwandishi huyo, Michael Drosnin, aliandika kwamba alijaribu kumwonya
waziri huyo mkuu kwa kipindi kinachozidi mwaka mmoja kwamba angeuawa
lakini hakusikiliza.
Vitabu vingine na makala nyingine
ambazo zimechapishwa zinadai kwamba ujumbe huo wa siri una uthibitisho
kamili kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu. Je, kuna ujumbe kama huo? Je,
ujumbe wa siri uwe msingi wa kuamini kwamba Biblia imepuliziwa na
Mungu?
Je, Ni Wazo Jipya?
Wazo la kwamba kuna ujumbe wa
siri katika maandishi ya Biblia si jipya. Ndilo wazo kuu la Kabala, au
mapokeo ya mafumbo ya Kiyahudi. Kulingana na walimu wa Kabala, yale
yanayoonekana kuwa maana ya maandishi ya Biblia kumbe si maana ya kweli.
Wanaamini kwamba Mungu alitumia herufi moja-moja za maandishi ya Biblia
ya Kiebrania kama ishara ambazo zikieleweka vizuri zinatokeza kweli
kubwa. Kwa maoni yao, kila herufi ya Kiebrania na mahali pake katika
maandishi ya Biblia iliwekwa na Mungu kwa kusudi fulani hususa.
Kulingana na Jeffrey Satinover,
mtafiti mmoja wa ujumbe huo wa siri wa Biblia, Wayahudi hao wa mafumbo
huamini kwamba herufi za Kiebrania zilizotumiwa kuandika masimulizi ya
uumbaji katika Mwanzo zina nguvu nyingi sana za mafumbo. Yeye aandika:
“Kwa kifupi, kitabu cha Mwanzo si ufafanuzi tu; ndicho chombo hasa cha uumbaji wenyewe, mfano halisi wa akili ya Mungu ikionyeshwa katika hali halisi.”
Rabi mmoja wa karne ya 13 wa
Kabala, Bachya ben Asher wa Saragossa, Hispania, aliandika juu ya herufi
za siri ambazo alifunuliwa aliposoma kila herufi ya 42 katika sehemu
fulani ya kitabu cha Mwanzo. Njia hiyo ya kuruka herufi kwa kufuata
utaratibu fulani eti kugundua ujumbe wa siri ndiyo msingi wa wazo la
kisasa la ujumbe wa siri wa Biblia.
Kompyuta “Zafunua” Ujumbe Huo
Kabla ya enzi ya kutumia
kompyuta, mwanadamu hakuwa na uwezo wa kuchunguza vizuri maandishi ya
Biblia kwa njia hiyo. Lakini, Agosti 1994, jarida moja la Statistical Science
lilichapisha makala moja ambamo Eliyahu Rips wa chuo cha Jerusalem’s
Hebrew University na watafiti wenzake walitokeza madai yaliyoshangaza
sana. Walieleza kwamba kwa kuondoa nafasi zote zilizoko kati ya herufi
na kuruka idadi ileile ya herufi za maandishi ya Kiebrania ya kitabu cha
Mwanzo, waligundua majina 34 ya marabi mashuhuri yakiwa ndani ya
maandishi hayo, pamoja na habari nyinginezo, kama vile tarehe zao za
kuzaliwa au kifo, zikiwa karibu na majina yao.*
Baada ya kufanya majaribio mara nyingi, watafiti hao walichapisha
uamuzi wao kwamba habari iliyotiwa kwenye Mwanzo haingeweza kutukia tu
yenyewe—hiyo ikiwa uthibitisho wa habari iliyopuliziwa ambayo ilifichwa
kwa makusudi iwe siri katika kitabu cha Mwanzo maelfu ya miaka
iliyopita.
Akitumia njia hiyo, mwandishi wa
habari, Drosnin, alifanya majaribio yake mwenyewe, akitafuta habari ya
siri katika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia ya Kiebrania. Kulingana
na Drosnin, alipata jina la Yitzhak Rabin katika maandishi ya Biblia kwa
utaratibu wa kuruka kila herufi 4,772. Akiwa amepanga maandishi ya
Biblia kwa mistari yenye herufi 4,772 kila mmoja, aliona jina la Rabin
(likisomwa kuelekea chini) likipitana na mstari mmoja (Kumbukumbu la Torati 4:42, unaoelekea upande) ambao Drosnin aliufasiri kuwa “muuaji ambaye ataua.”
Kumbukumbu la Torati 4:42
hasa linazungumzia mtu aliyeua bila kukusudia. Kwa hiyo wengi
wamechambua mbinu ya Drosnin isiyo na msingi, wakidai kwamba mbinu zake
zisizo za kisayansi zinaweza kutumiwa kupata ujumbe mwingine wowote kama
huo katika maandishi yoyote. Lakini Drosnin alijitetea, akisema: “Wale
wanaonichambua wakipata ujumbe unaohusu kuuawa kwa Waziri Mkuu katika
[kitabu] Moby Dick, nitakubaliana nao.”
Je, Ni Uthibitisho wa Upulizio?
Profesa Brendan McKay, wa Idara
ya Sayansi ya Kompyuta katika Chuo Kikuu cha Australia, alikubali mwito
wa Drosnin, akatumia kompyuta sana kuchunguza maandishi ya Kiingereza ya
kitabu Moby Dick.*
Akitumia ile mbinu iliyotajwa na Drosnin, McKay adai kwamba alipata
“matabiri” ya kuuawa kwa Indira Gandhi, Martin Luther King, Jr., John
F. Kennedy, Abraham Lincoln, na wengineo. Kulingana na McKay, aligundua
kwamba Moby Dick pia “ilitabiri” kuuawa kwa Yitzhak Rabin.
Akirudia maandishi ya Kiebrania
ya Mwanzo, Profesa McKay na wenzake pia wamepinga matokeo ya majaribio
ya Rips na wenzake. Walidai kwamba matokeo hayategemei ule ujumbe wa
siri bali wategemea mbinu za utafiti za watafiti hao—watafiti wenyewe
wakihusika hasa kwa kuingiza habari wanazotaka. Mjadala wa wasomi juu ya
jambo hili waendelea.
Suala jingine lazuka wakati
ambapo madai yanafanywa kwamba ujumbe kama huo wa siri ulifichwa
kimakusudi katika maandishi “sanifu” au “ya awali” ya Kiebrania. Rips na
watafiti wenzake wasema kwamba walifanya utafiti wakitumia “maandishi
sanifu yaliyokubaliwa ya [kitabu cha] Mwanzo.” Drosnin aandika: “Biblia
zote katika lugha ya awali ya Kiebrania ambazo zinapatikana sasa
zinafanana herufi kwa herufi.” Lakini, je, kweli zinafanana? Mbali na
maandishi “sanifu,” aina kadhaa za Biblia ya Kiebrania zinatumiwa leo,
zikitegemea hati-kunjo tofauti-tofauti za kale. Ingawa ujumbe wa Biblia
hautofautiani, hati-kunjo za awali hazifanani herufi kwa herufi.
Tafsiri nyingi leo zinategemea
Kodeksi ya Leningrad—ambayo ni hati-kunjo ya Kiebrania ya Wamasora iliyo
kamili na ya kale zaidi—iliyonakiliwa wapata mwaka wa 1000 W.K. Lakini
Rips na Drosnin walitumia maandishi tofauti, yale ya Koren. Shlomo
Sternberg, rabi wa Othodoksi aliye pia mtaalamu wa hesabu katika Chuo
Kikuu cha Harvard, aeleza kwamba Kodeksi ya Leningrad “yatofautiana na
chapa ya Koren iliyotumiwa na Drosnin kwa herufi 41 katika Kumbukumbu la
Torati pekee.” Hati-kunjo za Bahari ya Chumvi zinatia ndani sehemu za
maandishi ya Biblia zilizonakiliwa zaidi ya miaka 2,000 iliyopita. Mara
nyingi mwendelezo wa maneno katika hati-kunjo hizo hutofautiana sana na
maandishi ya baadaye ya Wamasora. Katika baadhi ya hati-kunjo hizo,
herufi ziliongezwa kwa wingi ili kuonyesha sauti za irabu, kwa kuwa
herufi za irabu hazikuwa zimevumbuliwa. Katika hati-kunjo nyinginezo,
herufi chache zilitumiwa. Ulinganishi wa hati-kunjo zote za Biblia
zilizoko waonyesha kwamba maana ya maandishi ya Biblia haijabadilika.
Lakini ulinganishi huo pia unaonyesha waziwazi kwamba mwendelezo na
idadi ya herufi zatofautiana kati ya hati-kunjo hizo.
Kutafuta ule unaosemekana kuwa
ujumbe wa siri kwategemea maandishi yasiyobadilika kabisa. Badiliko la
neno moja tu laweza kuharibu kabisa ule utaratibu—na ujumbe wowote ambao
ungekuwapo. Mungu amehifadhi ujumbe wake kupitia Biblia. Lakini
hajahifadhi kila herufi ikiwa vilevile, kana kwamba yuazingatia sana
mambo madogo-madogo kama mabadiliko ya mwendelezo katika karne
zilizopita. Je, jambo hilo halionyeshi kwamba hajaficha ujumbe fulani wa
siri katika Biblia?—Isaya 40:8; 1 Petro 1:24, 25.
Je, Tunahitaji Ujumbe wa Siri Katika Biblia?
Mtume Paulo aliandika wazi
kwamba “andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa
kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika
uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa
kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Si vigumu kutumia wala kuelewa ujumbe rahisi na wa wazi ulio katika Biblia, lakini watu wengi huamua kuupuuza. (Kumbukumbu la Torati 30:11-14) Unabii ambao unatolewa wazi katika Biblia ni msingi imara wa kuamini upulizio wake.* Tofauti na ujumbe wa siri, unabii wa Biblia hautegemei maoni ya mtu, na ‘hauchipuki kutokana na fasiri yoyote ya faragha.’—2 Petro 1:19-21.
Mtume Petro aliandika kwamba
“haikuwa kwa kufuata hadithi zisizo za kweli zilizotungwa kwa usanifu
mwingi kwamba tuliwafahamisha nyinyi juu ya nguvu na kuwapo kwa Bwana
wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 1:16)
Wazo la ujumbe wa siri wa Biblia lilianzishwa na mafumbo ya Kiyahudi,
yakitumia mbinu “zilizotungwa kwa usanifu” zinazoficha na kupotosha
maana ya wazi ya maandishi yaliyopuliziwa ya Biblia. Maandiko yenyewe ya
Kiebrania yalishutumu waziwazi utumizi kama huo wa mafumbo.—Kumbukumbu la Torati 13:1-5; 18:9-13.
Tuna furaha iliyoje kuwa na
ujumbe wa wazi wa Biblia na mafundisho yake, ambao unaweza kutusaidia
kumjua Mungu! Huo unafaa zaidi kuliko kujaribu kujifunza juu ya Muumba
kwa kutafuta ujumbe wa siri ambao unatokezwa na fasiri ya faragha na
mawazo yenye kutegemea utumizi wa kompyuta.—Mathayo 7:24, 25.
Kipengele: Habari mpya, Tuisome Biblia
0 Maoni