Kumfundisha Mtoto Habari za Mungu

Unknown | 3:44:00 PM | 0 Maoni

ken_drink

Watoto wanajifunza sana kutokana na jinsi watu waliowazunguka wanavyoishi/kuenenda. Vile vile wanajifunza kwa kuangalia picha na michoro ya aina mbalimbali. Njia hizi ndizo zinafaa kutumika wakati unamfundisha mtoto wa kuanzia mwaka mmoja habari za Mungu maana ndio anaweza kukuelewa zaidi. Ni vyema ukaanza na umri huu mdogo kuliko kusubiri akue zaidi ndio uanze kumfundisha habari za Mungu.

1. Omba na mtoto wako wakati wote, iwe chakula, asubuhi ukiwa unaondoka/ameamka, wakati wa kwenda kulala au hata wakati mnapotoka pamoja kwenda popote. Kwa kufanya hivi mara kwa mara taratibu naye ataanza kuona kuwa maombi ni kitu cha muhimu na kadiri anavyokuwa haitakuwa ngumu kumfundisha kuhusu umuhimu wa maombi. Nimeona jambo hili kwa mtoto wetu Kenneth, kwa sababu ya mazoea  ya kuomba pamoja amejenga tabia hiyo na hata kama sipo akipewa chakula lazima kwanza afunge macho na amumunye maneno kisha anasema ame ndipo anakula, vile vile anapoenda kulala mchana,  kwanza anamwambia dada  ‘ aomba’ maana kuwa anaomba kwanza ndipo alale. Biblia inasema mlee mtoto katika njia impasayo naye hataiacha hata atakapokuwa mzee Mithali 22:6.

2. Msimulie hadithi za biblia kwa njia ya kufurahisha huku ukiwa unamsomea biblia. Mwanzoni itakuwa ngumu kukuelewa lakini kadiri unavyoendelea na kurudia rudia mara kwa mara itakaa ndani yake na itamjengea tabia ya kusoma biblia ili ajue zaidi zile habari unazomsimulia pale atakapokuwa anajua kusoma. Mnunulie biblia ya watoto yenye hadithi fupi fupi za biblia na picha. Waweza pia tafuta Video CD au DVD za hadithi za biblia kwa watoto na kuangalia pamoja naye huku ukimsimulia, kwanza itakupa musa mzuri wa kukaa na kufurahi na mtoto wako na huku ukimfundisha habari za Mungu aliye hai.

3. Imba naye nyimbo za kumsifu Mungu hasa zile zinazopendwa na watoto. Mtoto tangia akiwa tumboni anapenda sana kusikia mtu akimuimbia hasa kama ni mzazi wake, sio lazima utenge muda wa kuanza kuimba na mtoto bali pale unapokuwa unamuogesha, unafua na yeye anacheza nk tumia muda huo pia kumuimbia nyimbo za Mungu huku ukimfundisha na yeye.

 Mtafutie CD za picha na sauti za watoto wanaomuimbia Mungu na mueleze kuwa wanaimba kwa furaha sababu wanamuimbia Mungu. Hii itampa hamasa ya kumuimbia Mungu kama watoto wenzie anaowaona na kuwasikia. Mwambie wanamwimbia Mungu sababu ni mwema, anatupenda, ametuumba, anatupa chakula, ametupa wazazi nk. ili aone uhalisia wa upendo wa Mungu.

4. Mfundishe kuonyesha shukrani pale mtu anapompatia kitu au kumtendea jambo jema. Hata kama hajui kuongea mwambie tu sema asante, mshukuru kwa sababu fulani, hii itamfundisha kuwa ukitendewa jambo ni lazima kuonyesha shukrani. Mfundishe kumshukuru Mungu kwa kuamka salama, kupata wazazi wa kumletea maziwa, kununuliwa toy mpya, kumuona bibi n.k. Moyo wa shurani utamsaidia kumjua Mungu zaidi na kwa hali hii atakuwa anatafuta mema ya kumshukuru Mungu kila siku.

5. Ishi maisha ya upendo, ukarimu na furaha wakati wote ili mtoto aone uhalisia wa Mungu katika maisha yako. Nenda naye kanisani na uwe unamwambia kwa nini huwa unaenda kanisani, kumshukuru Mungu, kumuomba Mungu, nk. Usisahau kumpa sadaka naye awe anatoa huku ukimweleza ni njia ya kumshukuru Mungu kwa vingi alivyotupatia.

Kumbuka kila mara kumkumbusha upendo wa Mungu, wema wa Mungu, ukuu wa Mungu. Muonyeshe vitu mbalimbali na kumwambia kuwa Mungu ameviumba(ameviweka) mfano ndege, wadudu, miti, maua, wanyama n.k. Ni vyema mtoto akafahamu habari kamili za Mungu kabla hajaanza shule, hii itakuwa ulinzi wake katika dunia hii ilivyojaa uharibifu.
Mungu atusaidie sana tunapowalea watoto wetu katika kweli ya Mungu. Amen.

Kipengele: , ,

KUHUSU NEEMA MBISE MINISTRY:
Ni Mchungaji na mwimbaji wa nyimbo za injili hapa Tanzania!

0 Maoni